Uzinduzi huu umefanyika leo na mgeni wa heshima alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Said Mecky Saddick na ulihudhuriwa na waendesha bodaboda,maofisa wa serikali,na askari wa kikosi cha usalama barabarani ambapo waendesha bodaboda walikabidhiwa vifaa vya kuwakinga wakati wa ajali na sare maalum za kuwatambulisha wanapokuwa kazini
Waendesha bodaboda watakaokuwa kwenye mpango huu muda wote watatakiwa kuwa wamevaa sare zilizoandikwa namba zao maalum za kuwatambulisha,kituo wanachoegesha pikipiki zao na namba maalumu ya kupiga wakati wakati wa dharura.
Waendesha bodaboda wataweza kuingia kwenye mpango huu wa bima ya kuwakinga na kupatiwa sare pindi watakapofuata utaratibu uliowekwa wa kujiunga kwa mujibu wa kanuni za kufanya biashara ya kuendesha pikipiki za wilaya wanazofanyia kazi.
Huduma hii imebuniwa kutokana na ongezeko la ajali za pikipiki na pia biashara hiyo kuhusishwa na vitendo vya uharifu mara kwa mara.Sare zitasaidia abiria kuwatambua waendesha bodaboda halisi wanaopaswa kuwakodisha na bima ya afya itawasaidia wakati wa majamnga ya ajali na kupoteza maisha.
Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Alternative Communication Edward Mgaya alisema “bima hii mpya iliyozinduliwa leo itawawezesha waendesha bodaboda kupata huduma za matibabu wakati wanapopatwa ajali au kulipa mafao familia zao wakati mhusika aliyekata bima anapopoteza maisha.Mchango wa bima hii kwa mwezi ni shilingi 3,000/- ambapo mwendesha bodaboda atakayejiunga na mpango huu atatakiwa kulipia shilingi 1,000/-ambapo fedha zinazoongezeka zitalipwa kwa ruzuku maalumu”
Alisema waendesha bodaboda watakaojiunga na mpango huu ni lazima kutumia vifaa vya kuwakinga vilivyotolewa ikiwemo kuvaa sare ili wapatapo ajali waweze kulipwa kwa mujibu wa taratibu za bima hii.
Akiongea kwa niaba ya Chama cha Waendesha Bodaboda,Bwana Bakari Sagalla aliipongeza Vodacom na Alternative Communication kwa kuja na ubunifu huu ambao umelenga kuwakinga waendesha bodaboda nchini kimaisha na kusaidia biashara hii kuwa na mpangilio maalumu tofauti na hivi sasa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania Rene Meza alisema “Tunaendelea kufanya kazi na wadau mbalimbali kutoa elimu ya usalama barabarani kwa jamii ya watanzania.Ushirikiano huu na kampuni ya Alternative Communication ni ubunifu wenye tija ambao utapunguza ajali za pikipiki na vitendo vya uharifu kutumia vyombo hivi”
Sare maalumun zilizotolewa zitawatofautisha waendesha bodabado halisi na wale wanaotumia kisingizio cha kubeba abiria na kujihusisha na vitendo vya uharifu.
Ushirikiano huu pia utatoa fursa kwa waendesha bodaboda watakaotaka kufanya biashara ya M-Pesa katika maeneo wanayofanyia kazi au kuitangaza huduma hiyo na watajengewa mazingira bora ya kufanya biashara hiyo.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Said Mecky Sadick ambaye alikuwa mgeni rasmi aliipongeza Vodacom na Alternative Communication kwa kuja na ubunifu huu muhumi wenye lengo la kupunguza ajali za pikipiki na kuboresha maisha ya waendesha vyombo hivyo na alizitaka taasisi nyingine na makampuni kuiga mfano huu na kuingia kwenye kampeni hii.
Mkuu wa Kitengo cha Elimu na Mafunzo kutoka Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani ACP Abel Swai alisema kuwa ajali za barabarani zimekuwa zikiongezeka na kusababisha vifo na ulemavu kwa wananachi wengi.Alisema ajali za bodaboda nyingi zinachangiwa na waendeshaji wake kutofuata sheria zan usalama barabarani na uzembe na aliwahimiza waendesha bodaboda kuchangamkia fursa ya mpango huu wa bima ambapo wataweza kupata vifaa vya kinga,bima na elimu ya usalama barabarani.
Baada ya mpango huu kuzinduliwa Dar es Salaam utafuatia mkoa wa mbeya na mikoa mingine nchini.Vodacom imekuwa mstari wa mbele kuunga mkono jitihada za serikali za kutoa elimu ya usalama barabarani kupitia kampeni yake ya ‘Wait to Send’ inayowahamasisha madereva kutotumia simu wanapokuwa wanaendesha vyombo vya moto.
No comments:
Post a Comment