HALI NI TETE, DAR YAKUMBWA NA MAFURIKO!

Baadhi ya nyumba zilizo bondeni katika eneo la Mkwajuni, Kinondoni jijini Dar.
Namna ambavyo soko la Sinza-Afrika Sana linavyoonekana kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha jijini Dar.
Mkazi wa Tandale kwa Tumbo akitoa maji yaliyojaa kwenye nyumba yake kufuatia mvua kali zinazoendelea kunyesha jijini Dar.
Wakazi wa Tandale kwa Tumbo na maeneo ya jirani wakipita kwa tabu katika njia hiyo kufuatia mvua ambazo zinaendelea kunyesha jijini Dar.
WAKATI mgomo wa mabasi ukimalizika juzi, wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wamekumbwa na adha nyingine, baada ya mvua kubwa zinazoendelea kunyesha kuleta madhara mbalimbali kijamii na kiuchumi.
Katika maeneo mbalimbali ambayo waandishi wetu walitembelea leo, walikuta baadhi ya wakazi wakitoa maji yaliyoingia ndani ya nyumba zao na sehemu za kufanyia bishara zao.
Baadhi ya wakazi wa maeneo ya Mwanayamala Mkwajuni maarufu kama ‘Bondeni’ wameonekana kutupia lawama Kampuni ya ujenzi ya Strabag kuwa ujenzi wao wa barabara ndio umechangia nyumba zao kuingiliwa na maji kwani mifereji iliyotengenezwa haikidhi uwezo wa kusafirisha maji kwa kasi maana ni midogo, badala yake maji hujaa na kupitisha juu kuelekea katika makazi yao.
Wakati huo huo waandishi wetu walifika maeneo ya Jangwani na kukuta baadhi ya nyumba zilizoko bondeni zikiwa zimezama majini, huku wakilalamika kutaka serikali iwasaidie, licha ya ukweli kwamba walishaambiwa siku nyingi kuhama mabondeni.

Wakati huo huo, eneo la soko la Sinza-Afrika Sana, waandishi wetu waliwakuta wafanyabiashara ndogondogo wakilaumu mifereji inayopitisha maji barabarani kuziba kufuatia uchafu unaotupwa na kuziba maji kufika hadi sokoni hali inayopelekea biashara zao kudoda kutokana na wateja kukosa sehemu ya kupita.

No comments:

Post a Comment