STARTIMES YAWAPIGA TAFU WANAFUNZI UHURU MCHANGANYIKO

Msanii wa Bongo Flava na balozi mpya wa kampuni ya StarTimes Tanzania, Nurdin Bilal au maarufu kama Shetta (kulia) akimkabidhi msaada wa vyakula mbalimbali Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko ya jijini Dar es Salaam, Bi. Anna Mshana (kushoto). Kampuni hiyo ilitembelea na kutoa msaada wa vyakula kwa wanafunzi wa shule hiyo ambayo ina kitengo kinachofundisha wanafunzi wenye ulemavu. Pamoja naye kutoka kushoto ni wafanyakazi wa kampuni hiyo Bi. Elena Liu na Bw. Richard Yan.
Msanii wa Bongo Flava na balozi mpya wa kampuni ya StarTimes Tanzania, Nurdin Bilal au maarufu kama Shetta akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati kampuni hiyo ilipotembelea na kutoa msaada wa vaykula kwa Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko ya jijini Dar es Salaam jana.
Dar es Salaam, Mei 6, 2015.
Katika kuijali jamii ya watanzania ambao ndio wateja wake wakubwa, kampuni ya usambazi na uuzaji wa ving’amuzi nchini, StarTimes Tanzania, imetembelea na kutoa msaada wa vyakula wenye thamani ya shilingi milioni 3.5 kwa wanafunzi wenye ulemavu, shule ya msingi Uhuru Mchanganyiko ya jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya vyakula vilivyotolewa shuleni hapo ni mchele zaidi ya kilo 200, unga zaidi ya kilo 150, mafuta ya kupikia, sukari, chumvi, sabuni za kupikia na vinginevyo.
Akizungumza baada ya kupokea masaada huo Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko, Bi. Anna Mshana alishukuru sana kwa msaada huo kwani wamekuwa wakishirikiana kwa karibu na StarTimes ni mara ya pili kwenda shuleni hapo.
“Hii ni mara ya pili kuja hapa kwani mara ya kwanza walituletea luninga na king’amuzi ambacho tunakitumia mpaka hivi leo. Hivyo StarTimes ni kama walezi wetu naweza kusema kwani tukiwa na tatizo tunawaona na kutusaidia. Mimi sina cha ziada zaidi ya kuwashakuru kwa moyo wao wa kutukumbuka kila wanapofanya shughuli zao.” Alisema Bi. Mshana
“Shuleni hapa tunawanafunzi wa kawaida lakini pia kuna walemavu wa ngozi (albino), , viziwi, vipofu, wenye ulemavu wa akili na ulemavu mwingine. Wanafunzi hawa tuna hapa, tunawafundisha na pia wana mabweni yao ambayo ndimo wanapokaa. Chakula ni kitu muhimu kwao kwani ndio kinawapa motisha ya kuhudhuria na kupenda kusoma zaidi. Hivyo msaada huu umekuwa mwokozi wetu mkubwa kwa wakati huu.” Alimalizia mwalimu mkuu huyo
Kwa upande wake akizungumza na wanafunzi na uongozi wa shule, Makamu wa Rais wa StarTimes Tanzania, Bi Zuhura Hanif amesema kuwa wanajisikia wenye wajibu mkubwa kusidia jamii inayowazunguka kwani wapo kwa ajili yao.
“StarTimes tunajisikia kuwajibika kwa jamii inayotuzunguka na ambao ndio wateja wetu katika shughuli zetu. Linakuwa si jambo la busara kuendesha shughuli zako huku hauna msaada wowote kwa jamii yako. Leo tumejumuika hapa na msanii huyu wa muziki wa kizazi kipya kushirikiana kuwafariji wanafunzi hawa wenye uhitaji maalumu ili waweze kusoma.” Alisema Bi. Hanif
“Najua hata kama ningekuwa mimi ni mzazi wa mmojawapo wa watoto hawa ningefurahi kuona kuwa kumbe kuna watu wanawajali na kuwatambua watoto wao. Suala hili linatia faraja na hata kuwapa moyo wazazi ambao wana watoto wa namna na kuwaficha majumbani mwao kwa kudhani kuwa hawawezi kufanya jambo lolote. Ningependa kuwaambia kwamba wasiwanyime watoto wao fursa ya elimu au ya kujichanganya na watoto wenzao kwani kuzaliwa mlemavu si sababu ya kutoweza kufanya jambo lolote.” Aliongezea
“Hivyo basi wanafunzi na uongozi wa Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko nawaomba mpokee kidogo hiki tulichwaletea ili kiweze kuwasaidia katika shughuli zenu za kimasomo. Napenda kuwatoa hofu kuwa msisite kutushirikisha pale mnapoona tunaweza kuwasaidia. Natoa wito kwa watu wengine kujenga utaratibu wa kuwakumbuka na kuwasiadia watu wenye uhitaji maalumu kama watoto hawa. Ninaamini watanzania ni wakarimu na watu wa kusaidiana siku zote.” Alihitimisha Bi. Hanif

No comments:

Post a Comment