JINSI YA KUISHI NA MWANAMKE MZURI BILA PRESHA

Kibinadamu tunasema hakuna mwanamke mzuri na mbaya. Wote ni sawa na yule ambaye unamuona kwako ni mzuri, huenda kwa mwenzako akawa mbaya.Hata hivyo, wapo wanawake ambao kiuhalisia ni wazuri na hata wenzao wanakiri kwamba Mungu kawapendelea.

Uzuri ninaouzungumzia hapa ni ule wa sura na umbo. Wapo ambao wamejaaliwa kuwa na figa bomba kiasi kwamba kila mwanaume anatamani ampate.
Linapozungumziwa suala la kuoa, wanaume wengi sasa hivi hawaangalii sura wala umbo, tabia imekuwa kigezo cha msingi. Ndiyo maana unaweza kushangaa wapo wanawake wazuri tu huko mtaani lakini hawapati wanaume wa kuwaoa, kwa nini? Kwa sababu hawana tabia nzuri.
Lakini pia sasa hivi wapo wanawake wengi wazuri na wenye tabia nzuri ila imekuwa ngumu kwao kupata wachumba. Ukifuatilia utagundua kuwa, kuna dhana kwamba kuoa mwanamke mzuri ni kujipa presha.Ukweli ni kwamba si kila mwanamke mzuri ukimuoa atakupa presha, bali yapo mambo ya kuzingatia ili uweze kuishi kwa amani na furaha.
YANAYOMHUSU MKEO
Awe amekupenda kwa dhati
Unapomuoa mwanamke ambaye wewe umempenda kwa dhati na unaamini ni mzuri kwako, chunguza kama na yeye uko moyoni mwake.
Hii ni kwa sababu unaweza kuingia naye kwenye ndoa lakini kama hana mapenzi na wewe ni rahisi kukufanyia vitimbwi pale atakapompata ambaye moyo wake umemridhia.
Ajiheshimu
Ukioa mwanamke mzuri ambaye hata yeye anajijua kuwa ni mzuri, zungumza naye kuhusu suala la kujiheshimu. Asiwe na utani na wanaume, ajue nguo za stara za kuvaa, ajue yeye ni mke wa mtu na kutowapa wanaume wakware nafasi ya kummendea.
Asiwe na tamaa za kijinga
Ni vyema ukazungumza naye mara kwa mara kuhusu maisha. Ujue kuna kupata na kukosa! Ajue kuwa pesa hazina thamani mbele ya utu. Atambue kwamba wapo watakaojifanya wanampenda, wakampa pesa lakini kumbe wana nia mbaya.
Ajue thamani ya ndoa
Ni vyema mwanamke utakayemuoa akajua thamani ya ndoa. Awe tayari kuitunza ndoa yake kwa gharama yoyote. Akumbuke pia kwamba, wapo wazuri zaidi yake ambao mpaka leo wanaililia ndoa lakini wasipate wanaume wa kuwaoa.
Uzuri wake si chochote
Huenda kweli ni mzuri na marafiki zake wanakubali hilo lakini yeye ajue kabisa kwamba uzuri wake siyo tiketi ya kumfanya adumu kwenye ndoa. Wapo wazuri ambao waliachika na leo hii wanatanga na njia wasipate hata wapenzi wa kuzugia.

Itaendelea wiki ijayo.

No comments:

Post a Comment