UNA UHAKIKA GANI KAMA MPENZI WAKO HAWEZI KUNASWA NA WAJANJA, KWA KIPI?

NIkweli mapenzi ni imani, yaani kuamini kwamba uliyenaye anakupenda hata kama ukweli unaweza usiwe hivyo. Wengi walio na wapenzi wanajiaminisha kwamba wanavyowapenda wenza wao ndivyo wananvyopendwa.

Pia wapo ambao wanaamini kwamba eti kwa namna wanavyoonesha mapenzi yao, hata kwa dawa hawawezi kusalitiwa. Utamsikia mwanamke akisema; “bwana wangu mimi kwangu hapindui, ananipenda sana na hawezi kunisaliti’.
Mtu anayesema maneno hayo anajipa imani na ukifuatilia unaweza kukuta huyo anayesema hivyo, mpenzi wake ni kiwembe ile mbaya.
Ni wanaume wangapi ambao wewe unawajua wake zao wanawaamini sana lakini kumbe wanasalitiwa sana kwa siri? Ni wanaume wangapi, tena wengine wakiwa marafiki zako ambao wake/wapenzi wao wanawaamini sana lakini wanasifika kwa kupenda totozi?
Watu hao wako huko mtaani, tena wengi tu na yawezekana hata mpenzi wako unayemuamini sana si muaminifu, anajifanya ni mtu mpole, anayejiheshimu, asiye na mawazo ya kukusaliti lakini kumbe akiwa mbali na wewe, ni hatari.
Lakini sasa, kama ukweli uko hivyo, tuna sababu ya kuishi kwa hofu tukihisi kwamba wapenzi wetu si waaminifu? Hapana! Kuishi kwa wasiwasi ni kujipa presha za bure na za kujitakia.
Ni kweli kwa ulimwengu wa sasa hakuna mtu anayeweza kumuamini mpenzi wake kwa asilimia zote lakini kisaikolojia unatakiwa kumuamini kwa asilimia zote huyo uliyenaye.Hata kama yapo anayofanya akiwa mbali na upeo wa macho yako, iwe ni yeye na Mungu wake lakini kwa kuwa hujawahi kumfumania wala kuona ishara zozote za kwamba anakusaliti, jenga imani naye.
Imani unayojipa ni kwa lengo la kujipa amani ya moyo, uishi kwa furaha na kujiweka mbali na presha zisizokuwa na msingi.Ila sasa, nawashangaa sana wale ambao wanajiaminisha kwamba wapenzi wao hawawezi kuwasaliti kwa namna yoyote. Unajua kwa nini nawashangaa?
Ni kwa sababu huko mtaani kuna vishawishi vingi, wapo wasichana wazuri sana ambao wao hawajali kwamba huyu ni mume wa mtu, watamtega kwa kila namna ili wamnase.Wapo ma-handsome na mapedeshee ambao wakimtaka mwanamke yeyote watafanya kila njia wampate. Sasa wewe ambaye uko kwenye uhusiano unafanya yapi ya kumfanya mwenza wako ayashinde majaribu?
Maana usikae na kusema mpenzi wako hakusaliti, lazima uwe na sababu za kusema na kujiaminisha hivyo. Je, umejenga mazingira ya mpenzi wako kukuona wewe ndiyo wewe wengine takataka? Kama hujafanya hivyo usijidanganye, kaa ukijua wajanja wanakumegea penzi lako.
Ninachotaka ukijue leo kupitia makala haya ni kwamba, huko mtaani kuna mitego mingi kwa wapenzi kiasi kwamba ni wachache sana wanaoweza kuikwepa. Mfanye mpenzi wako awe kati ya wale ambao hawanasi kirahisi.
Mpende, mjali, mthamini, mpe penzi linalostahili lakini pia zungumza naye kila mara kwamba, hao wazuri huko nje wanaomtaka, hawana mapenzi ya kweli. Ni walaghai tu wanaomtamani ila mwenye mapenzi ya kweli kwake ni wewe.
Pia zungumza naye kuhusu magonjwa, mueleze kabisa kwamba, hata kama kwa tamaa zake atakusaliti huko gizani, magonjwa yatakuja kumuumbua.
Naamini ukifanya hivyo, hata kama hutawaambia watu kwamba mpenzi wako hawezi kukusaliti, wewe mwenyewe utakuwa na imani kubwa kwa kuwa umemuandaa kukwepa vishawishi. Ni hayo tu kwa leo, tukutane tena wiki ijayo kwa mada nyingine.

No comments:

Post a Comment